Monday, July 22, 2013

WAVAA VIMINI WAPIGWA MARAFUKU KUINGIA HOSPITALI YA MKOA WA DODOMA



MGANGA Mkuu wa Hospitali ya Mkoa wa Dodoma, Dk Ezekiel Mpuya amesema tangazo lililotolewa hospitalini hapo la kuwataka watu kuvaa mavazi ya heshima wanapoingia hospitalini hapo lilikuwa likihusu watumishi wa hospitali hiyo na si wananchi wa kawaida.


Akizungumzia suala hilo juzi, Dk Mpuya alisema kuwa Katibu wa Hospitali hiyo alitoa tangazo hilo kimakosa hali ambayo ilisababisha walinzi kuzuia watu waliovaa ‘ovyo’ kuingia hospitalini hapo.
“Uongozi wa Hospitali unaomba radhi kwa usumbufu waliopata wagonjwa na wananchi waliofika hospitalini hapo kwani tangazo lilitolewa kimakosa na Katibu kwani lilikuwa likiwahusu watumishi pekee na si wananchi,” alisema Dk Mpuya.


Kwa mujibu wa tangazo hilo, Hospitali ya Mkoa wa Dodoma iliweka masharti ya uvaaji ambapo mavazi yaliyopigwa marufuku ni sketi fupi, fulana zisizo na mikono nguo za kubana pamoja na Jeans.


Juzi kulitokea kutoelewana kati ya walinzi na watu waliokuwa wakitaka kuingia hospitalini hapo na kuzuiwa kutokana na aina ya mavazi waliyokuwa wamevaa.

No comments: